UONGOZI wa klabu ya Azam umeamua kumrejesha kocha Sterwart Hall kwa ajili ya kuiongoza timu hiyo kwenye msimu ujao wa ligi na michuano ya kimataifa.
Habari za uhakika zilizopatikana kutoka ndani ya uongozi wa Azam Dar es Salaam jana, zilisema uongozi umeona Hall bado ana nafasi kwenye klabu hiyo.
“Ni kweli Hall anarudi Azam na jana (juzi) tumemalizana naye, anatarajia kuanza kazi rasmi Juni 15 siku ambayo timu itarudi kambini… maana kwanza ametuomba akatoe notisi kwenye ofisi yake Sunderland."
Hall ni mwajiriwa katika Kituo cha Michezo cha Kidongo Chekundu kinachojengwa kwa ushirikiano na kampuni ya umeme ya Symbion na klabu ya Sunderland ya Uingereza kwa ajili ya kuinua kipaji.
Mtoa habari wetu aliliambia gazeti hili kuwa kocha Hall anarudi kwenye nafasi yake ya ukocha mkuu huku George Nsimbe na Dennis Kitambi wakiwa wasaidizi wake.
“Mambo yote yameshakamilika Hall anasubiriwa kuanza kazi tu na wasaidizi wake watakuwa Nsimbe na Kitambi, hatutawabadilisha hao,” alisema. Hall anarudi Azam kwa mara ya tatu sasa.
Aliitumikia katika vipindi viwili tofauti, ambapo mara ya kwanza ikiwa ni katika msimu wa mwaka 2012/2013 alipoiongoza kumaliza nafasi ya pili kwenye Ligi Kuu Bara na kupata nafasi ya kushiriki michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika.
Sababu za kuondoka msimu huo ilikuwa ni kutoelewana na uongozi baada ya kocha huyo kumpanga Mrisho Ngassa (aliyekuwa Azam wakati huo) katika mechi ya fainali ya Kombe la Kagame Julai 2012, ambapo Azam ilicheza na Yanga na kufungwa kwa mabao 2-0.
Hall alirudi tena Azam katika msimu wa mwaka 2013/2014 na kuiongoza timu hiyo katika mechi zote za raundi ya kwanza kabla ya uongozi wake kutangaza kusitisha mkataba naye kwenye mechi ya mwisho ya raundi ya kwanza iliyochezwa Chamazi na kutoka sare ya mabao 3-3 dhidi ya Mbeya City.
Mcameroon Joseph Omog ndiye aliyechukua mikoba ya Hall na kuiongoza Azam katika mzunguko wa pili msimu huo, ambao timu hiyo ilicheza bila kupoteza mechi na kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu Bara kwa mara ya kwanza.
Omog na msaidizi wake, Ibrahim Shikanda waliiongoza Azam katika msimu wa ligi wa mwaka 2014/2015 kabla ya kufutwa kazi Februari mwaka huu baada ya Azam kutupwa nje ya michuano ya kimataifa ya Ligi ya Mabingwa Afrika na timu ikawa chini ya Nsimbe na Kitambi, ambao waliiongoza kumaliza nafasi ya pili katika ligi.
Katika hatua nyingine, Azam imemuongezea mkataba wa miaka miwili mchezaji wake Salum Abubakar huku ikimalizana na Erasto Nyoni na Said Morad ambao wanatarajiwa kusaini mkataba muda wowote.
Aidha, timu hiyo imesitisha mkataba wake na David Mwantika na imeshamlipa stahiki zake zote na kwamba yupo huru baada ya kutoridhika na kiwango chake.
“Azam ilisaini mkataba wa miaka miwili na Mwantika na unatarajia kumalizika Novemba, baada ya majadiliano ikaonekana bora kusitisha mkataba na mchezaji huyo ili awe huru na kutafuta timu nyingine,” alisema kiongozi huyo. Mwantika alijiunga na Azam FC akitokea Prisons ya Mbeya
Comments
Post a Comment