MDHIBITI na Mkaguzi Mkuu mpya wa Hesabu za Serikali (CAG), Profesa Mussa Assad, ameamua kuiorodheshea Serikali mapendekezo yote ya mtangulizi wake, Ludovic Utouh, ambayo hayajatekelezwa na Serikali tangu 2008 na kusisitiza sasa yatekelezwe.
Katika mapendekezo ya mwaka 2009/2010, Profesa Assad, amelalamikia kitendo cha Serikali kuendelea kuruhusu mwanya wa mgongano wa maslahi, kwa kuendelea kuteua wabunge kuwa wajumbe wa bodi za mashirika na taasisi za umma.
“Bunge ndio chombo cha juu kinachowakilisha wananchi na chenye majukumu ya kutathimini utendaji kazi wa Serikali, ikiwa ni pamoja na mashirika na taasisi nyinginezo za umma kupitia kamati za kudumu za Bunge.
“Ili kuepuka mgongano wa kimaslahi, nasisitiza mapendekezo yangu kuwa, wabunge hawastahili kuteuliwa kuwa wajumbe wa bodi za wakurugenzi katika mashirika na taasisi nyinginezo za umma, kwani wana jukumu la kusimamia mashirika hayo,” amesema Profesa Assad.
Posho sawa Akielezea mapendekezo ya mwaka 2008/2009 ambayo hayajafanyiwa kazi, Profesa Assad ameitaka Serikali kuhakikisha kuwa kuna uwiano katika marupurupu wanayopata menejimenti na bodi za wakurugenzi za taasisi za umma.
“Hii inatokana na ukweli kuwa rasilimali wanazotumia kama posho za vikao, ada za bodi za wakurugenzi na nyinginezo, ni rasilimali za umma,” alisema Profesa Assad.
Alisema hatua ya Serikali kuanzisha Bodi ya Uwiano wa Mishahara na Marupurupu, itasaidia kuondoa tofauti zilizopo sasa za kuongeza ufanisi na uwajibikaji katika mashirika na taasisi nyinginezo za umma.
Wanaodaiwa Bodi ya Mikopo Kuhusu kutorejeshwa kwa mikopo ya Sh bilioni 51, iliyokopwa na wanafunzi wa zamani wa vyuo vikuu, ambao sasa hivi ni waajiriwa au wamejiajiri, Profesa Assad aliishauri Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu kuwachukulia hatua za kisheria waajiri na wakopaji binafsi, ambao hawatoi ushirikiano.
Alitaka hatua hiyo ichukuliwe kwa kuzingatia Sheria Namba 9 ya Bodi hiyo ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu, Kuhusu mkopo uliokopeshwa katika Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu wa Sh bilioni 54 kutoka Mfuko wa Pensheni kwa Wanafunzi wa Umma (PSPF), alitaka Serikali irejeshe mkopo wote na riba.
Adhabu TPA Kuhusu mapendekezo ya mwaka 2010/2011, Profesa Assad alirejea ukaguzi wa mwaka huo, uliobaini kuwa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) ilifanya ununuzi wa dharura milioni 13 bila idhini kutoka kwa Mlipaji Mkuu wa Serikali. “Sina taarifa ya hatua zilizochukuliwa kuhusu suala hilo la ununuzi wa dharura wa Mamlaka ya Bandari Tanzania,” amesema.
Katika mwaka huo huo, Profesa Assad alihoji kwa nini Waziri wa zamani wa Kilimo, Hifadhi ya Chakula na Ushirika, ameendelea kukaa katika nyumba ya Bodi ya Sukari Tanzania, iliyopo Kiwanja 482 Barabara ya Bray Masaki.
Mgogoro wa UDA Profesa Assad pia aliendelea kuhoji uuzwaji wa hisa za Shirika la Usafiri Dar es Salaam (UDA), uliofanywa na Bodi ya Wakurugenzi wa shirika hilo bila kupata kibali cha Serikali. Alisema hisa za UDA zilikuwa na thamani ya Sh 744.79 kila hisa Oktoba 2009 na ilipofika Novemba 2010 thamani ya kila hisa ikawa Sh 656.15.
Kwa mujibu wa Profesa Assad, katika uuzwaji wa hisa hizo, Bodi ya Wakurugenzi iliamua kutoa punguzo la asilimia 60 kwa kila hisa, bila kuwepo kwa sababu ya kufanya hivyo.
Profesa Assad alieleza kuwa Mlipaji Mkuu wa Serikali alipoulizwa, alisisitiza kuwa hatambui uuzwaji wa hisa hizo na Serikali inaandaa mapendekezo ya kuuza asilimia 49 ya hisa za UDA, na itafikisha mapendekezo hayo katika Baraza la Mawaziri.
“Majibu haya (ya Mlipaji Mkuu wa Serikali), hayasemi chochote kuhusu mustakabali wa hisa ambazo zilishauzwa na hatua zilizochukuliwa dhidi ya wakurugenzi wa Bodi ya Wakurugenzi wa UDA,” alisema.
Benki ya Azania Profesa Assad pia alihoji inakuwaje mashirika ya pensheni yameanzisha Benki ya Azania, halafu benki hiyo ikaanzishwa kama kampuni binafsi na kuachwa kuwa katika orodha ya mashirika yanayosimamiwa na Msajili wa Hazina.
Kwa mujibu wa Profesa Assad, benki hiyo ambayo awali iliitwa 1st Adili Bancorp Limited, wanahisa wake ni Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) hisa asilimia 34.8, Mfuko wa Pensheni wa PPF hisa asilimia 30.1, Mfuko wa Pensheni wa PSPF hisa asilimia 17.2, Mfuko wa Pensheni wa LAPF hisa 14.2, Benki ya Maendeleo ya Afrika Mashariki (EADB) hisa 2.3 na wafanyakazi wa Benki ya Azania na wanahisa wengine wenye asilimia 1.4.
CAG katika hilo aliweka wazi kuwa mifuko ya pensheni, ndiyo yenye hisa nyingi sawa na asilimia 96.3, na hivyo ndiyo yenye nguvu ya kutoa miongozo na kusimamia benki hiyo na kwa kuwa mifuko yote ya pensheni inamilikiwa na Serikali, ni wazi benki hiyo ni mali ya Serikali.
Kutokana na mazingira hayo, Profesa Assad alihoji kwa nini benki hiyo haijawahi kuwasilisha hesabu Zake katika ofisi ya CAG tangu 1995 ilipoanzishwa, kwa ajili ya ukaguzi kama Katiba inavyotaka.
Comments
Post a Comment