Skip to main content

Kima cha chini mishahara chapanda

RAIS Jakaya Kikwete ameahidi kuongeza mishahara ya wafanyakazi kuanzia Julai mwaka huu, ili walau kima cha chini kikaribie Sh 315,000 ambazo Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (Tucta) limekuwa likiipigia kelele kwa muda mrefu.

Kikwete alisema hayo alipokuwa akihutubia wananchi waliohudhuria sherehe za Siku ya Wafanyakazi Duniani, zilizofanyika kitaifa kwenye viwanja vya CCM Kirumba jijini Mwanza jana.

Rais Kikwete alisema, “Ongezeko lililoko ni dogo sana lakini si haba. Na mwaka huu tutaongeza mshahara kufikia Sh 315,000 kima cha chini na kama hakitafikia, tutaangalia mahesabu yetu kwa nini, angalau ikaribie hiyo”.

Rais Kikwete alisema serikali imechukua hatua za makusudi za kuongeza mshahara kila mwaka tangu alipoingia madarakani mwaka 2005 ambapo kima cha chini alikuta Sh 65,000 na amekipandisha na sasa kimefika Sh 265,000 ambayo ni zaidi ya mara nne.

Kuhusu kauli iliyotolewa na vyama vya upinzani vinavyounda Ukawa kuwa serikali imepanga kusogeza uchaguzi mkuu usifanyike Oktoba mwaka huu ili kumuongezea muda Rais Kikwete aendelee kutawala, amejibu na kusema hana mpango huo.

“Nimesikia wazee (viongozi wa Ukawa) wanasema serikali haina mpango wa kufanya uchaguzi. Urais wangu hauna mpango wa kufanya hivyo. Aibu! Sijui maneno haya wameyatoa wapi...” alisema.

Kwa upande mwingine alisema serikali imeendelea kupunguza kiwango cha kodi wanayotozwa wafanyakazi (PAYE) mwaka hadi mwaka. Alikuta asilimia 18.5 na kimeshuka katika utawala wake na kufikia asilimia 12.

“Na mwaka huu tutapunguza sijui tutafikia asilimia 9 kama mnavyotaka ila tutakapofikia si pabaya,” alisema Kikwete bila kutaja kiwango cha asilimia kitakachopunguzwa.

Akizungumzia mshahara katika sekta binafsi, alisema kima cha chini hupangwa na bodi za mishahara za kisekta na kwamba majadiliano yalikuwepo ambayo yalipandishwa kutoka Sh 48,000 hadi Sh 700,000 kulingana na sekta.

Aidha alikitaka Chama cha Waajiri (ATE) kuliweka kwenye ajenda suala la waajiri wanaolipa chini ya kiwango watakapokwenda kukutana naye.

Alisema katika kipindi cha uongozi wake aliahidi ajira milioni moja lakini hadi anaondoka madarakani zaidi ya ajira milioni 2.6 zinapatikana kutoka serikalini pamoja na sekta binafsi.

Kikwete alionya baadhi ya waajiri ambao hawalipi viwango vilivyokubaliwa vya mishahara, kwa kusema hilo sio jambo la kiungwana na linahuzunisha. “Waajiri hufikia makubaliano ya bodi za kisekta katika ulipaji wa mshahara.

Tusikubali watu hawa waendelee kuhujumu haki za wafanyakazi. “Naomba mamlaka husika tusikubali watu hawa wakaendelea kudhulumu haki za wafanyakazi,” alisema Rais Kikwete.

Pia alisema wanajishughulisha kwa kadiri ya uwezo wao kutafuta matatizo yanayowakabili wafanyakazi, yale ambayo hayakupatiwa ufumbuzi si kwa sababu ya udogo wa dhamira bali ugumu wa tatizo lenyewe.

“Ambayo sijasema leo naendelea na nitaendelea kuyashughulikia mpaka nitakapokabidhi kwa huyo atakayekuja. Tutaendelea na Wizara ya Kazi na Ajira na ofisi ya takwimu kukuza ajira Tanzania,” alisema.

Alisisitiza kuwa rais ajaye atamkabidhi orodha ya yale mambo ambayo ni kiporo na anayojua mwenyewe na atatoa ushirikiano kwa rais ajaye.

Katika sherehe hizo Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (Tucta), Nicholus Mgaya alitaja madai waliyoyatoa kwa rais, kuwa makato ya kodi ni makubwa.

Mgaya alisema mwaka jana PAYE ilipungua hadi kufikia asilimia 12, lakini mategemeo yao ifikie asilimia 9 mwaka huu. Mgaya aliwataka wafanyakazi kutumia kura yao ipasavyo katika uchaguzi mkuu kwa kuchagua viongozi wanaojali tabaka la wafanyakazi.

Na jijini Dar es Salaam,

Wafanyakazi wamelitaka Bunge kutopokea na kujadili bajeti za taasisi za umma, ikiwemo wizara mbalimbali zilizopelekwa bungeni bila kuzingatia sheria inayotaka kuwashirikisha wafanyakazi kupitisha bajeti za taasisi zao.

Sheria hiyo ya ajira na uhusiano kazini namba sita ya mwaka 2004 inataka kuwashirikisha wafanyakazi kupitisha bajeti zao kwa kutumia mabaraza ya wafanyakazi.

Wafanyakazi hao walisema hayo pamoja na kudai kima cha chini cha mshahara kuwa Sh 720,000 badala ya Sh 100,000 au 250,000 kilichopo sasa katika hotuba yao iliyosomwa na Katibu wa Chama cha Wafanyakazi wa Migodi, Nishati, Ujenzi na Kazi Nyingine (Tamico) kanda ya Dar es Salaam na Pwani, Charles Mgashi.

Hotuba hiyo ilitolewa katika maadhimisho ya siku ya wafanyakazi iliyoadhimishwa kimkoa katika Uwanja wa Uhuru, huku mgeni rasmi akiwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadiki.

Akizungumza katika hafla hiyo na kujibu baadhi ya maombi hayo, Sadiki alikiri kuwa ni ukweli usiopingika mshahara hautoshi na sehemu nyingine za kazi mazingira ni magumu lakini pamoja na changamoto, wafanyakazi wamekuwa wakifanya kazi kwa tija na ubunifu.

Na huko Zanzibar,

Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi (SMZ), Dk Ali Mohamed Shein amewataka wanasiasa kuacha kuwadanganya vijana kwamba wana uwezo wa kuwapatia ajira na kusisitiza dunia yote sasa inakabiliwa na tatizo hilo ambalo linatokana na kuyumba kwa uchumi.

Akizungumza katika kilele cha sherehe za siku ya wafanyakazi duniani zilizofanyika kisiwani Pemba katika uwanja wa Makonyo, alisema nchi maarufu zenye uchumi mkubwa duniani zimeyumba na kukabiliwa na tatizo la ajira ikiwemo za Ulaya na kutolea mfano Denmark.

“Nawaomba wanasiasa muache tabia ya kuwadanganya vijana kwamba mna uwezo mkubwa wa kuwapatia ajira vijana si kweli...si Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wala Serikali ya Muungano ajira ni tatizo kubwa,” alisema.

Alisema Serikali ya Mapinduzi ya awamu ya saba tangu ilipoingia madarakani imefanya kazi kubwa ya kuzalisha ajira kupitia taasisi zake pamoja na sekta binafsi ambazo zimepewa nafasi kubwa ya kufanya kazi nchini.

Kwa mfano alisema katika mwaka 2010 jumla ya ajira za vijana 25,019 zimepatikana katika taasisi mbalimbali Unguja na Pemba, huku katika sekta binafsi ajira zilizopatikana ni 4,850.

Aidha alisema kima cha chini cha mshahara kiliongezeka kutoka Sh 100,000 katika mwaka 2011 na kufikia Sh 125,000 pamoja na posho kwa wafanyakazi wake huku kiwango hicho kikipanda na kufikia Sh 150,000 sawa na asilimia 20.

Aidha katika hotuba yake alisema Serikali haitovumilia kikundi cha wanasiasa kuanzisha vurugu kwa kisingizio cha kutekeleza demokrasia na kuongeza kwamba uchaguzi unasimamiwa na taasisi zilizopewa jukumu hilo kwa mujibu wa katiba na sheria.

“Nataka niwahakikishie wafanyakazi na wananchi kwa ujumla kwamba Serikali zote mbili, mimi na Rais Jakaya Kikwete tutasimamia amani na utulivu kuelekea uchaguzi mkuu kwa lengo la kuona wananchi wanaishi katika mazingira ya utulivu,” alisema.

Imeandikwa na Grace Chilongola, Mwanza, Khatib Suleiman, Zanzibar na Theopista Nsanzugwanko na Lucy Ngowi, Da

Comments

Popular posts from this blog

Rais Wa Burundu "Apinduliwa"......Ndege Yake Jana Ilishindwa Kutua Burundi na Kuamua Kurudi Tanzania

Nchini Burundi, aliyekua mkuu wa majeshi Jenerali Godefroid Niyombare ametangaza Jumatano Mei 13 kuwa rais wa nchi hiyo Pierre Nkurunziza amepinduliwa madarakani. Meja Generali Niyombareh alisema wamechukua hatua hiyo baada ya watu wa Burundi kukataa kwa kinywa kipana awamu ya tatu ya urais wa Nkurunziza. Jenerali huyo aliyetimuliwa na Nkurunziza mwezi februari alisema kuwa Nkurunziza alishindwa kuheshimu mwafaka wa amani mbali na sheria za kimataifa. Wakati  Mapinduzi  hayo  yakitangazwa, Rais Nkurunziza alikuwa  nchini Tanzania kujumuika na viongozi wa kanda  ya Afrika Mashariki kutafuta suluhu ya mgogoro wa Burundi tangu Nkurunzinza atangaze nia yake ya kuwania awamu ya tatu. Baada  ya  tangazo  la  kupindulikwa  kwake, Rais  huyo  alipanda  ndege  kurejea  nchini  kwake  licha  ya  tangazo  la  kufungwa  kwa  mipaka  yote  na  viwanja  vya...

Diamond Amuita Jokate Makombo...."Mwacheni Ali Kiba Ajilie Makombo"

Mkali wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond’ amemuita mpenzi wake wa zamani Jokate Mwegelo kuwa ni makombo na kudai kama zilipendwa huyo anatembea na hasimu wake Ali Kiba, hakuna jipya kwani anakula makombo. Diamond ametoa kauli hiyo Jumatano iliyopita wakati mwanahabari wetu alipotaka kujua anajisikiaje kuona wapenzi wake wa zamani Jokate na Wema Sepetu ‘Madam’ wanamuunga mkono Ali Kiba. Pamoja na kudaiwa kuwa Jokate ana uhusiano wa ‘kimalovee’ na Ali Kiba na mwenyewe kutokubali, ameungana na Wema kuendesha kampeni ya nguvu kwenye mitandao ya kijamii kuhamasisha watu wampigie kura Kiba kwenye Tuzo za Kili 2015 kwa kile kinachoelezwa kuwa ni kampeni ya kuuangusha ufalme wa Diamond kimuziki. Baada ya mwanahabari wetu kuujua ‘mchezo huo’ uliopamba moto kama moto wa kifuu mitandaoni ndipo alipomuuliza Diamond anauzungumziaje ambapo kwanza alikiri kuufahamu na kudai ameudharau maana hauna jipya. “Hamna jipya waache waendelee kumpigia...

Gharama za kupima ardhi kupunguzwa

SERIKALI imesema katika mwaka ujao wa fedha itapunguza gharama za upimaji ardhi kwa zaidi ya nusu ili kuwawezesha wanachi kupima maeneo yao, hali ambayo inaonekana itapunguza migogoro ya ardhi. Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi wakati wa ziara mkoani hapa kwa ajili ya kutatua migogoro ya ardhi ambayo imedumu kwa miaka mingi. Akizungumza na watendaji wa sekta mbalimbali wa mkoa wa Tabora, Waziri Lukuvi alisema Wizara itapunguza kwa zaidi ya nusu, gharama za upimaji ardhi ili kila mwananchi aweze kupima eneo lake na kupata hati ya umiliki. Lukuvi aliongeza kuwa serikali pia itaweza kukusanya kwa wingi kodi ya pango la ardhi, hivyo kuongeza mapato ambayo yataisaidia serikali katika kufanikisha shughuli za maendeleo. Pamoja na kupunguza gharama hizo, Lukuvi aliwaonya maofisa ardhi kuacha tabia ya kuendesha shughuli za serikali kwa kukiuka taratibu, akitolea mfano wa maofisa hao kupima viwanja juu ya viwanja suala ambalo limekuwa lina...