BAADA ya Simba kupata ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Azam FC juzi, Kocha wa timu hiyo, Goran Kopunovic licha ya kuiombea Yanga iifunge timu hiyo ya Chamazi, ametamba kuwa Simba ndio ‘mabingwa’ msimu huu.
Ushindi huo unaifanya Simba kutofautiana kwa pointi moja na Azam FC, ingawa wapinzani wao hao wana faida ya michezo miwili ambayo kama itashinda, itachukua nafasi ya pili wakati Simba imebakiza mchezo mmoja pekee.
Simba inashika nafasi ya tatu ikiwa na pointi 44, moja nyuma ya Azam FC, wakati wakiwania kumaliza nafasi ya pili nyuma ya bingwa mpya, Yanga na kupata tiketi ya kushiriki michuano ya kimataifa mwakani.
Akizungumza baada ya mchezo huo uliochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Kopunovic alisema uwezekano wa kuchukua nafasi ya pili utategemea na matokeo ya mchezo wa Yanga na Azam FC utakaochezwa kesho.
“Hatima yetu ya kushika nafasi ya pili itategemea na mchezo wa Yanga, kwa hiyo tunasubiri tuone kwani tunatamani tushiriki michuano ya kimataifa mwakani,” alisema kocha huyo raia wa Serbia.
Akizungumzia mchezo huo dhidi ya Azam FC, Kopunovic alikisifu kikosi chake kwa kucheza vizuri na kufanikiwa kupata matokeo ambayo waliyataka.
Alisema kikosi chake kilionesha kuimarika kwani kila mchezaji aliyeingia alionesha juhudi ya kutaka kufanya vizuri. Licha ya kuiombea Azam FC ifungwe, kocha huyo alijitapa kuwa wao ndio mabingwa kwa vile walifanikiwa kuifunga Yanga na Azam msimu huu.
“Yanga wanasema wao ni bora na Azam vile vile, lakini niseme kuwa sisi ni bora kuliko wote kwa sababu tumewafunga, kwa hiyo tu naweza kusema ni mabingwa,” alitamba kocha huyo mwenye vituko akiwa uwanjani.
Katika Ligi Kuu msimu huu, Simba ilitoka sare ya bao 1-1 na Azam FC katika mzunguko wa kwanza kabla ya kushinda juzi, wakati Simba ilitoka sare ya 0-0 na Yanga katika mzunguko wa kwanza kabla ya vijana wa Jangwani kuzama kwa bao 1-0 katika marudiano, katika mechi ya kwanza ya Kopunovic akiwa na Simba.
Kocha huyo wa Simba hakusita kuipongeza Yanga kwa hatua waliyofika kwanza katika kuchukua ubingwa wa ligi, lakini pia kufanya vizuri kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika.
Alisema Yanga walionesha mchezo mzuri dhidi ya Etoile Sportive du Sahel kwani walijitahidi kwa uwezo wao.
Naye Kocha wa Azam FC, George Nsimbe alisema hawaangalii nyuma walipofungwa, kwani wanajipanga kwa mchezo dhidi ya Yanga ili kuondoka na pointi tatu.
Inahitaji pointi tatu kuifuta Simba kupanda ndege mwakani. Nsimbe alionesha matumaini kuwa iwapo watajitahidi katika mchezo huo watachukua nafasi ya pili.
Comments
Post a Comment