KLABU ya Yanga imesema inatarajia kufanya usajili wa wachezaji wazuri wa kimataifa kwa ajili ya kukisaidia timu yao ya soka kufanya vizuri katika Ligi ya Mabingwa Afrika mwakani.
Akizungumza na waandishi wa habari jana Dar es Salaam, Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Yanga, Jerry Muro alisema wataangalia wachezaji wengine wazuri ambao watasaidia sio tu katika michuano ya kimataifa, bali ikiwezekana kutetea taji hilo kwa msimu ujao.
Muro alisema hawatarajii kufanya usajili wa wachezaji kutoka Simba kwani wamejifunza kutokana na makosa. “Usajili tutafanya kwa wachezaji wengine wa kimataifa hivyo hatutarajii uongozi wetu utasajili wachezaji kwa watani zetu Simba, hata kama ni mzuri kwa kiasi gani au ni malaika, hatutafanya wala hatutarajii,” alisisitiza Muro.
Kuhusu ni wachezaji gani wataachwa, alisema ni mapema kusema kwa sasa kwani hilo ni suala la benchi la ufundi. Alisema hajui ni nani ataachwa kwani hayo hujulikana baada ya kumalizika kwa msimu na kisha wakishapewa ripoti ya benchi hilo ndipo watajua wanaohitajika na wasiohitajika.
Mkuu huyo wa Habari pia alikanusha taarifa za usajili wa Simon Msuva na Haruna Niyonzima Simba kwamba ni za uzushi na kuwataka wanachama wa klabu hiyo kutosikiliza taarifa hizo.
Pamoja na hayo, alizungumzia mchezo wao wa kimataifa dhidi ya Etoile Sportive du Sahel uliochezwa mwishoni mwa wiki iliyopita mjini Sousse nchini Tunisia kuwa licha ya kutolewa, wamechukulia kama ni sehemu ya changamoto kujipanga kwa ajili ya Ligi ya Mabingwa mwakani.
“Tumeyakubali matokeo, tumejifunza mambo mengi na tunachukulia mapungufu yetu kwa ajili ya kujipanga,” alisema. Yanga ilitolewa baada ya kufungwa bao 1-0 na hivyo kutupwa nje kwa jumla ya mabao 2-1 baada ya sare ya bao 1-1 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Aprili 18, mwaka huu.
Aidha, timu hiyo ya Jangwani tayari imetawazwa bingwa wa Tanzania Bara kwa mara ya 25 baada ya kufikisha pointi 55 ambazo haziwezi kufikiwa na timu nyingine 13 zinazoshiriki ligi msimu huu. Leo inacheza na Azam FC
Comments
Post a Comment