CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimetangaza tarehe za wagombea wa nafasi mbalimbali za uongozi kuchukua na kurejesha fomu, ambapo kwa nafasi ya Rais, zitatolewa Julai 20 na kurejeshwa Julai 25.
Mwenyekiti wa Taifa wa chama hicho, Freeman Mbowe alisema jijini Dar es Salaam jana, tarehe hiyo na za madiwani na wabunge kuchukua fomu, zimepitishwa na Kamati Kuu ya CHADEMA kwenye mkutano uliofanyika kwa siku mbili.
Kwa mujibu wa Mbowe, wabunge wataruhusiwa kuanza kuchukua fomu za kugombea nafasi hiyo kwa vipindi viwili tofauti, ambapo Mei 18 itakuwa siku ya watakaotaka kugombea Ubunge kwenye majimbo, ambayo kwa sasa chama hicho hakina wagombea.
Aidha, ilielezwa kuwa siku hiyo wanaowania nafasi ya Ubunge wa Viti Maalum nao wataruhusiwa kuchukua fomu na kuzirejesha na wanaowania Ubunge kwenye majimbo yasiyo na wabunge wa CHADEMA ifikapo Juni 25.
“Julai 6 itakuwa ni siku ya kuchukua fomu za ubunge katika majimbo ambayo chama chetu kina wabunge na Julai 10 ndio zitatakiwa kurejeshwa”, Mbowe alisema na kuongeza kuwa, Mei 18 itakuwa siku ya kuchukua fomu za Udiwani kwenye Kata ambazo chama chake hakina Madiwani, zitakazotakiwa kurejeshwa Juni 25.
Kwa upande wa kata ambazo kuna madiwani wa chama hicho, imeelezwa kuwa, fomu za Udiwani zitaanza kutolewa Julai mosi na kurejeshwa Julai 10, kuruhusu uteuzi wa mwisho wa wagombea Udiwani na wale wa Viti Maalum.
Kutokana na ratiba iliyotolewa na chama hicho, uteuzi wa mwisho wa wagombea Ubunge utafanyika Agosti mosi na Agosti 2, wakati Baraza Kuu la Taifa la chama hicho litakaa Agosti 3 na Mkutano Mkuu kuendeshwa Agosti 4.
Mbali na hayo, Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk Willibrod Slaa alisema muungano wao na vyama vingine vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), umeamua kutumia mkakati wa kuachiana nafasi katika maeneo ambayo mgombea anayependekezwa anaonekana kuyamudu ili kuishinda CCM.
Mjumbe wa Jopo la Wataalamu katika UKAWA ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya CHADEMA, Profesa Mwesiga Baregu alisema mkakati mwingine wanaoufikiria kuutekeleza hapo baadae ni wa kuifanya UKAWA iwe chama kimoja.
Wakati akijibu swali la gazeti hili kwenye mkutano na wanahabari alisema, “Wazo hilo tunalo lakini kwa sasa hatuwezi kuua vyama vyetu kwa kuwa bado tunajijenga, kuendelea kufahamiana na kuelewana”. “…Ikibidi hapo baadae, kabla ya uchaguzi mkuu, tutajiunga na kuwa chama kimoja tu, yaani UKAWA bila CHADEMA, NCCR-Mageuzi, NLD na CUF,” alisema
Comments
Post a Comment