Skip to main content

Mchungaji Gwajima Avamiwa.....Apigwa Panga Kichwani na Kulazwa ICU

MCHUNGAJI wa Kanisa la Ufufuo na Uzima jijini Mwanza, Samson Gwajima na Ofisa wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Amin Neigwa, wamevamiwa na majambazi ambao wamewajeruhi vibaya kwa kuwakata mapanga vichwani.

Tukio hilo lilitokea usiku wa kuamkia jana katika Mtaa wa Lyila, Kata ya Buhongwa, Wilaya ya Nyamagana, jijini Mwanza.

Akizungumza kwa taabu na mwandishi wetu akiwa wodini kwenye Hospitali ya Rufaa ya Bugando (BMC), alikolazwa kwa matibabu, Neigwa, alisema akiwa sebuleni nyumbani kwake na mkewe, ghafla walimuona msichana wa kazi aliyekuwa nje akichota maji, akiingia ndani kwa kasi na kukimbilia chumbani.

Alisema wakati akitahamaki kilichotokea, watu wanaosadikiwa kuwa majambazi waliingia ndani wakiwa na silaha za jadi kama mapanga, nyundo, vitu vyenye ncha kali na kutaka fedha.

"Walikuwa sita na baadhi yao walifunika sura zao kwa vitambaa, walinitaka niwape pesa...nilipata ujasiri wa kumrukia mmoja wao aliyekuwa na panga na kumkaba ndipo wengine wakanishambulia kwa kutumia silaha zao hadi nikapoteza fahamu," alisema.

Aliongeza kuwa, wakati wanamshambulia wengine walikuwa wanamlazimisha mkewe awape pesa lakini aliwakatalia na baadaye aliamua kuwapa sh. 10,000 ambayo ilikuwepo wakaichukua.

"Kelele nilizopiga wakati tumevamiwa zilisikika kwa majirani ambao walijitokeza ndipo wavamizi wakakimbia," alisema Neigwa ambaye alijeruhiwa kichwani ambapo hadi jana alikuwa akitokwa na damu masikioni.

Baada ya watu hao kukimbia, walienda kuvamia nyumbani kwa Mchungaji Gwajima na kumjeruhi kichwani kwa panga ambapo hivi sasa amelazwa katika hospitali hiyo kwenye Chumba cha Wagonjwa Wanaohitaji Uangalizi Maalumu (ICU).

Mchungaji Gwajima ni kaka wa Kiongozi wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Askofu Josephat Gwajima, ambaye alivamiwa alipokuwa amelala na familia yake eneo la Lyila na kulazimishwa kutoa fedha.

Akizungumza na mwandishi wetu, Mchungaji wa kanisa hilo, John Kiula,  alisema Mchungaji Gwajima alivamiwa usiku ambapo baadhi ya mashuhuda walidai baadhi ya meno yake yameng'oka.

"Hadi sasa bado hajajitambua, tumetoka kwenye kipimo cha CT-Scan lakini majibu bado hatujapewa tumeambiwa yakiwa
tayari watatujulisha," alisema Mchungaji Kiula.

Mkuu wa Idara ya Dharura hospitalini hapo, Dkt. Derick David, alikiri kuwapokea majeruhi hao usiku na kusema Mchungaji Gwajima alifikishwa akiwa na hali mbaya zaidi kuliko Neigwa.

"Gwajima ana jeraha kubwa kwenye paji la uso ambalo ni kama sentimita mbili hadi tatu kwa urefu kwenda ndani, kipimo cha X-Ray kimeonesha hajapasuka mfupa ila hali yake si nzuri.

"Hadi sasa bado hajitambui, tunatarajia kumfanyia kipimo kikubwa cha CT-Scan ambacho kitaonyesha ameumia kiasi gani lakini Neigwa anaendelea vizuri ingawa naye anahitaji kupimwa na CT-Scan ili kuona majeraha yake kama amepata athari ndani ya kichwa, tunaendelea kuokoa maisha yao," alisema.

Kamanda wa Polisi mkoani humo, Naibu Kamishna wa Polisi, Charles Mkumbo, alikiri kutokea kwa matukio hayo na kuahidi kuyatolea ufafanuzi ambapo baadhi ya watu wamekamatwa wakihusishwa na matukio hayo.

"Mkuu wa Upelelezi Mkoa na timu yake walikuwa wanaendelea na uchunguzi, wakiukamilisha nitalizungumzia kwa undani na kuwataja walioshikiliwa, baadhi ya majambazi hao wametambuliwa na majirani," alisema.

Comments

Popular posts from this blog

Rais Wa Burundu "Apinduliwa"......Ndege Yake Jana Ilishindwa Kutua Burundi na Kuamua Kurudi Tanzania

Nchini Burundi, aliyekua mkuu wa majeshi Jenerali Godefroid Niyombare ametangaza Jumatano Mei 13 kuwa rais wa nchi hiyo Pierre Nkurunziza amepinduliwa madarakani. Meja Generali Niyombareh alisema wamechukua hatua hiyo baada ya watu wa Burundi kukataa kwa kinywa kipana awamu ya tatu ya urais wa Nkurunziza. Jenerali huyo aliyetimuliwa na Nkurunziza mwezi februari alisema kuwa Nkurunziza alishindwa kuheshimu mwafaka wa amani mbali na sheria za kimataifa. Wakati  Mapinduzi  hayo  yakitangazwa, Rais Nkurunziza alikuwa  nchini Tanzania kujumuika na viongozi wa kanda  ya Afrika Mashariki kutafuta suluhu ya mgogoro wa Burundi tangu Nkurunzinza atangaze nia yake ya kuwania awamu ya tatu. Baada  ya  tangazo  la  kupindulikwa  kwake, Rais  huyo  alipanda  ndege  kurejea  nchini  kwake  licha  ya  tangazo  la  kufungwa  kwa  mipaka  yote  na  viwanja  vya...

Diamond Amuita Jokate Makombo...."Mwacheni Ali Kiba Ajilie Makombo"

Mkali wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond’ amemuita mpenzi wake wa zamani Jokate Mwegelo kuwa ni makombo na kudai kama zilipendwa huyo anatembea na hasimu wake Ali Kiba, hakuna jipya kwani anakula makombo. Diamond ametoa kauli hiyo Jumatano iliyopita wakati mwanahabari wetu alipotaka kujua anajisikiaje kuona wapenzi wake wa zamani Jokate na Wema Sepetu ‘Madam’ wanamuunga mkono Ali Kiba. Pamoja na kudaiwa kuwa Jokate ana uhusiano wa ‘kimalovee’ na Ali Kiba na mwenyewe kutokubali, ameungana na Wema kuendesha kampeni ya nguvu kwenye mitandao ya kijamii kuhamasisha watu wampigie kura Kiba kwenye Tuzo za Kili 2015 kwa kile kinachoelezwa kuwa ni kampeni ya kuuangusha ufalme wa Diamond kimuziki. Baada ya mwanahabari wetu kuujua ‘mchezo huo’ uliopamba moto kama moto wa kifuu mitandaoni ndipo alipomuuliza Diamond anauzungumziaje ambapo kwanza alikiri kuufahamu na kudai ameudharau maana hauna jipya. “Hamna jipya waache waendelee kumpigia...

Gharama za kupima ardhi kupunguzwa

SERIKALI imesema katika mwaka ujao wa fedha itapunguza gharama za upimaji ardhi kwa zaidi ya nusu ili kuwawezesha wanachi kupima maeneo yao, hali ambayo inaonekana itapunguza migogoro ya ardhi. Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi wakati wa ziara mkoani hapa kwa ajili ya kutatua migogoro ya ardhi ambayo imedumu kwa miaka mingi. Akizungumza na watendaji wa sekta mbalimbali wa mkoa wa Tabora, Waziri Lukuvi alisema Wizara itapunguza kwa zaidi ya nusu, gharama za upimaji ardhi ili kila mwananchi aweze kupima eneo lake na kupata hati ya umiliki. Lukuvi aliongeza kuwa serikali pia itaweza kukusanya kwa wingi kodi ya pango la ardhi, hivyo kuongeza mapato ambayo yataisaidia serikali katika kufanikisha shughuli za maendeleo. Pamoja na kupunguza gharama hizo, Lukuvi aliwaonya maofisa ardhi kuacha tabia ya kuendesha shughuli za serikali kwa kukiuka taratibu, akitolea mfano wa maofisa hao kupima viwanja juu ya viwanja suala ambalo limekuwa lina...