MFUNGAJI bora wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, Simon Msuva ameomba klabu yake Yanga SC imuuze kwa bei wakati akitakiwa na klabu ya Bidvest Wits ya Afrika Kusini.
Msuva amerejea juzi jioni Dar es Salaam baada ya siku tatu za kuwa Afrika Kusini kwa mipango ya kujiunga na klabu hiyo ya Ligi Kuu nchini humo.
Habari zaidi zinasema kuwa Bidvest Wits wameridhika na uwezo wa Msuva na wanataka kufungua majadiliano na klabu yake, Yanga SC ili kumsajili.
Msuva amebakiza mwaka mmoja katika Mkataba wake Yanga SC na Wits iko tayari kutumia si zaidi ya dola za Kimarekani 100,000 (Sh milioni 200) kukamilisha mpango huo.
Msuva aliondoka Dar es Salaam Jumatano wiki hii akiwa tayari ameipa Yanga SC ubingwa wa Ligi Kuu msimu huu, huku pia akiwa anaongoza kwa mabao 17, lakini inasemekana aliondoka bila kuuaga uongozi wake.
Mchezaji huyo alikosa mechi mbili za mwisho dhidi ya Azam FC wakati Yanga ikilala 2-1 na dhidi ya Ndanda ya Mtwara timu hiyo ikafungwa tena 1-0. Msuva alijiunga na Yanga mwaka 2012 akitokea timu ya Moro United ya Morogoro.
Comments
Post a Comment