Published on Wednesday, 13 May 2015 00:29
Written by Lucas Raphael, Tabora
Hits: 120
ASKARI Polisi watatu wa Kikosi cha Kuzuia Ghasia (FFU) mkoani Tabora, wamefikishwa mahakamani, akiwemo mkuu wa kikosi hicho, Mrakibu Msaidizi wa Polisi (ASP), Bhoke Julius Bruno.
Wote wanatuhumiwa kwa upotevu wa bunduki nane aina ya SMG, mali ya Jeshi la Polisi. Wengine waliopandishwa kizimbani mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mkoa wa Tabora, Issa Magori ni Koplo Idd Abdalah na Mwinyi Gonga, wote wa kikosi cha FFU, Tabora.
Akiwasomea mashitaka, Wakili wa Serikali, Juma Masanja aliiambia mahakama hiyo kuwa watuhumiwa wote watatu wanakabiliwa na shitaka moja la kutochukua tahadhari stahiki katika utunzaji wa silaha.
Alidai watuhumiwa hao, walitenda kosa hilo kati ya Aprili na Mei mwaka jana wakiwa waajiriwa wa Jeshi la Polisi, Kikosi cha Kutuliza Ghasia mkoani Tabora.
Wakili Masanja alidai watuhumiwa wakiwa Kikosi cha FFU Tabora kwa pamoja, walishindwa kutumia njia za kiusalama katika utunzaji wa silaha na matokeo yake bunduki nane aina ya SMG, zikaingia katika mikono ya watu ambao hawajaidhinishwa kwenye umiliki wake.
Watuhumiwa wote watatu walikana shitaka hilo na walinyimwa dhamana baada ya Wakili wa Serikali kupinga wasipewe kwa maelezo kwamba kuwepo kwao nje, kutaingilia upelelezi wa upatikanaji wa silaha hizo.
Kutokana na ombi hilo la serikali, Mahakama iliamuru watuhumiwa warudishwe mahabusu hadi Mei 21 mwaka huu, kesi hiyo itakapotajwa tena
Comments
Post a Comment