TAASISI ya Mifupa na Mishipa ya Fahamu (MOI) imepokea msaada wa kifaa cha kufanyia upasuaji chenye thamani ya Sh milioni 700 kutoka Chuo Kikuu cha Tiba cha Weill Cornell cha nchini Marekani.
Msaada huo umetolewa na chuo hicho ikiwa ni sehemu ya ushirikiano kati ya taasisi ya MOI.
Akizungumza jana Meneja Ustawi na Uhusiano wa taasisi hiyo, Almas Jumaa, alisema kifaa hicho kitatumika kufanya upasuaji wa ubongo, uti wa mgongo, mishipa ya fahamu na mifupa.
Alisema kifaa hicho kimeingia chumba cha upasuaji jana tayari kwa matumizi ya upasuaji kwa kushirikiana na wataalamu kutoka Chuo cha Weil Cornell.
“Wataalamu kutoka Chuo cha Cornell watatoa mafunzo ya vitendo kwa wataalamu wa taasisi ya MOI kwa kutoa huduma ya matibabu na upasuaji kwa wagonjwa kwa kutumia kifaa hicho.
“Tunatarajia kufanya upasuaji kwa wagonjwa 24 kwa muda wa siku tatu na upasuaji utakaofanyika ni wa kesi kubwa ambazo awali tulikuwa tunapeleka wagonjwa nje ya nchi kwa matibabu,” alisema Jumaa.
Alisema msaada walioupata ni kutokana na ushirikiano mzuri kati ya taasisi hiyo na chuo hicho hali itakayosaidia kuongeza ufanisi wa utoaji huduma na uwezo wa kuhudumia wagonjwa wengi.
Alisema wagonjwa wenye matatizo ya mishipa ya fahamu wamekuwa wakiongezeka kila siku na kwa sasa wanapokea wagonjwa 35 mpaka 40 kwa siku.
Alisema kwa sasa taasisi hiyo ina vifaa vya kutosha na ushirikiano na Chuo cha Cornell utaongeza ujuzi katika matumizi ya vifaa hivyo na kutoa huduma bora.
Comments
Post a Comment