Published on Thursday, 14 May 2015 00:07
Written by Sifa Lubasi, Dodoma
Hits: 783
SHIRIKA la Umeme nchini (TANESCO) linakusudia kupanga viwango vipya vya malipo ya umeme vitakavyotoa unafuu kwa taasisi hiyo na wadau wake endapo vyombo vinavyohusika, ikiwamo EWURA vitaidhinisha.
Hayo yalisemwa na Mkuu wa Idara ya Mipango Mikakati kutoka Tanesco Makao Makuu, Patrick Sankara katika Mkutano ulioandaliwa na Tanesco Makao Makuu na kufanyika Dodoma mkoani hapa.
Mkutano huo ni mwendelezo wa mikutano ya shirika hilo na wateja wake wenye lengo la kupata maoni ya watumiaji wake na kuzijua changamoto zitakazokuwepo baada ya Tanesco, kuanzia mpango wa kugawa viwango vya bei ya umeme kulingana na muda wa matumizi.
Alisema wale watakaokubadili muda wa matumizi watapatiwa punguzo maalumu kwenye viwango vyao.
Alisema matumizi ya umeme kwa sasa hupanda ghafla kuanzia saa 12:00 jioni hadi saa 4:00 usiku na kusababisha msukumo wa umeme kutoka katika vyanzo vyake kupungua na kusababisha Tanesco kuwasha mashine za ziada kufidia mzigo huo.
Akiwasilisha mada katika mkutano huo iliyohusu “Viwango vya muda wa matumizi ya Umeme”, Sankara alisema kutokana mahitaji hayo Tanesco inaingia gharama kubwa kuhakikisha inakidhi matakwa ya wateja wake.
“Gharama zote za kufidia matumizi haya ya ziada ni za Tanesco hivyo tunadhamiria kuja na mpango wa kuwashawishi wateja wakubwa kuhamisha muda wa matumizi yao kutoka saa za jioni na kuja muda wa asubuhi na mchana ambapo matumizi si makubwa sana,” alisema.
Akichangia katika majadiliano hayo Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Chiku Gallawa aliishauri Tanesco Mkoa wa Dodoma, kubuni utaratibu mpya wa kuwahudumia wateja wake ili kupunguza malalamiko na kukuza mahusiano mema.
Naye Kaimu Meneja wa Tanesco Kanda ya Kati, Joel Kuandika aliuambia mkutano huo kuwa wamepokea mapendekezo ya wateja hao na kuahidi kuyashughulikia ipasavyo.
Wakichangia mada hizo, baadhi ya watumiaji hao wakubwa walikubaliana na Tanesco kuhusu utaratibu mpya, lakini baadhi yao walionesha wasiwasi endapo Tanesco itaweza kusimamia utekelezaji wake kwa haki na umakini
Comments
Post a Comment