KLABU ya Yanga inatarajiwa kufanya uchaguzi Mkuu Julai 12 mwaka huu ambapo nafasi za Mwenyekiti , Makamu Mwenyekiti na Wajumbe zitawaniwa.
Awali uchaguzi huo ulikuwa ufanyike mwaka jana lakini baadhi ya wanachama walimwomba Mwenyekiti anayemaliza muda wake Yusuf Manji kuendelea kuwania tena nafasi hiyo kitu ambacho kilimlazimu kuwaomba wanachama hao asogeze mbele uchaguzi ili apate muda wa kufikiria ombi lao.
Akizungumza na gazeti hili Katibu Mkuu wa Kamati ya Uchaguzi ya Yanga Francis Kaswahili, aliwataka watu mbalimbali wenye mapenzi ya dhati na klabu hiyo kujitokeza kuwania nafasi hizo kwa lengo la kuipa mafanikio zaidi klabu hiyo.
“Jambo hili ni la kikatiba na wala halina mjadala, tunataka Yanga iwe na viongozi ambao watatokana na utashi wa Wanayanga ni matumaini ya Kamati ya Uchaguzi kwamba hapatatoka mtu mwingine wa kutaka kuvunja misingi ya Katiba,”alisema Kaswahili.
Alisema lengo la kutangaza tarehe ya uchaguzi mapema ni kutaka kupata viongozi wapya ambao watapata muda mzuri wa kuiandaa timu kwa ajili ya kutetea ubingwa wao wa bara msimu ujao na kufanya vizuri katika michuano ya Ligi ya Mabingwa ambayo mwakani.
Kaswahili alisema fomu za kuwania uongozi kwenye klabu yao zitaanza kutolewa keshokutwa kwa kuzingatia taratibu na kanuni ambazo zitawekwa kwa nia njema ya kuhakikisha klabu yao inapata viongozi bora.
Mara ya mwisho Yanga ilifanya Uchaguzi wake Mkuu Julai 18,2010 ambapo Lloyd Nchunga alichaguliwa kuwa Mwenyekiti na Delvis Mosha alichaguliwa katika nafasi ya Makamu Mwenyekiti huku wajumbe wakiwa ni Charles Mgondo, Ally Mayay, Mzee Yusuf na Theonest Rutashobolwa, Titus Ossoro, Sara Ramadhani, Mohamed Binda na Salum Rupia.
Lakini baadhi ya viongozi hao walijiuzulu nyadhifa zao na hivyo ikalazimika kufanyika uchaguzi mdogo Julai 15,2012 kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee na Manji alichaguliwa kuwa Mwenyekiti na Clement Sanga akichaguliwa kama Makamu Mwenyekiti na nafasi za Wajumbe wakachaguliwa Aaron, Nyanda, George Manyama, Abdallah Bin Kleb na Valentine Katabalo
Comments
Post a Comment