Skip to main content

Upinzani Burundi Wawaonya Marais EAC

WAKATI marais wa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) wakitarajiwa kukutana  Dar es Salaam leo kujadili mzozo wa  Burundi, wapinzani wa Rais Pierre Nkurunziza, wameapa kwa kusema kuwa ni lazima kiongozi huyo ang’atuke  madarakani.

Pamoja na hali hiyo pia wameonya kuwa silaha zinazozagaa kwa wanamgambo nchini humo zikusanywe kwa vile  ni hatari hata kwa usalama wa nchi jirani.

Akizungumza na waandishi wa habari  Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa Vuguvugu linaloendesha maandamano nchini humo, Chauvineau Mugwengezo, alisema kutano wa wakuu wa nchi za EAC ni lazima uzingatie suala hilo na yanayoendelea nchini mwao.

Mkutano huo unatarajiwa  kuhudhuriwa na Rais Paul Kagame (Rwanda), Uhuru Kenyatta (Kenya), Yoweri Museveni (Uganda) pamoja na Rais anayelalamikiwa kwa kutaka kuwania tena muhula wa tatu wa uongozi kinyume cha katiba ya Burundi, Pierre Nkurunziza.

Mugwengezo  alisema mkutano huo ambao utakuwa chini ya Mwenyekiti wa EAC Rais Jakaya Kikwete, lazima uhakikishe unaweka mazingira ya uchaguzi nchini Barundi kwa kuwashirikisha wanasiasa wote wa taifa hilo washiriki kwa ukamilifu.

Mwenyekiti huyo wa Vuguvugu la maandamano Burundi  alisema masharti mengine ni kuachiwa raia wote waliokamatwa na kuwekwa gerezani kwa sababu ya kufanya maandamano pamoja na kurudishwa  viongozi wa siasa waliokimbia nchini humo kwa kuhofia kuuawa kwa sababu ya kumpinga Rais Nkurunziza.

Alisema pia ni lazima Serikali ya Burundi ikubali kuwanyang’anya silaha zote wanamgambo wa Imbonerakure nchini humo.

“Watumie mbinu zote, ziwe za siasa ama kidplomasia, wahakikishe Nkurunziza anaondoka baada ya mihula yake miwili.

“Huo wa tatu ni kuvunja Katiba ya nchi na mkataba wa Arusha ambao Julius Nyerere na Nelson Mandela walihakikisha unafikiwa na ukaipa Burundi amani kwa miaka 10 sasa,” alisema.

Alisema mkataba wa Arusha na Katiba ya nchi hiyo hairuhusu mihula mitatu kwa kiongozi yeyote atakayetawala  Burundi.

“Hausemi kuwa uwe umechaguliwa na wananchi wala wabunge, unasema utawala uwe wa mihula miwili, lazima hili liheshimiwe.

“Hata kwenye Katiba ya nchi yetu inaanza kwa maneno; ‘Kwa kuzingatia Mkataba wa Arusha’, hii ina maana kila kitu kinazingatia mkataba wa Arusha,”   alisema Mugwengezo.

Alisema nchi za Ulaya, Amerika, Umoja wa Mataifa (UN) na mataifa mengine, yamempa ushauri Rais Nkurunziza lakini bado hataki kuusikia.

Mugwengezo alisema  hivi sasa  maelfu ya watu wameikimbia nchi hiyo  kutokana na kuhofia usalama wao, hasa ikizingatiwa kuwa wanamgambo wa Imbonerakure wanaua raia.

“Hawa wanamgambo wa Imbonerakure wanaweza kumchapa bakora hata ofisa wa jeshi na hakuna anayewazuia.  Silaha zilizo mikononi mwao hawa wana mgambo zinatishia hata usalama wa nchi za jirani ikiwamo Tanzania, lazima silaha hii zitoke mikononi mwao,” alisema.

Kiongozi huyo alimtuhumu Rais Nkurunziza kuwa anawasaidia wanamgambo  wa Imbonerakure hali ambayo inachangia kuvuruga amani ya nchi hiyo.

Alisema baada ya kufuatilia mazungumzo ya marais hao yatakayofanyika Dar es Salaam, watarudi  Burundi kuungana na wananchi wanaoendeleza maandamano.

Burundi  imeingia kwenye machafuko baada ya CNDD-FDD kumteua  Nkurunziza awania urais kwa muhula wa tatu  na  hadi sasa watu zaidi ya 10 wamefariki dunia kutokana na mapambano yanayoendelea kati ya waandamanaji na polisi.

Comments

Popular posts from this blog

Rais Wa Burundu "Apinduliwa"......Ndege Yake Jana Ilishindwa Kutua Burundi na Kuamua Kurudi Tanzania

Nchini Burundi, aliyekua mkuu wa majeshi Jenerali Godefroid Niyombare ametangaza Jumatano Mei 13 kuwa rais wa nchi hiyo Pierre Nkurunziza amepinduliwa madarakani. Meja Generali Niyombareh alisema wamechukua hatua hiyo baada ya watu wa Burundi kukataa kwa kinywa kipana awamu ya tatu ya urais wa Nkurunziza. Jenerali huyo aliyetimuliwa na Nkurunziza mwezi februari alisema kuwa Nkurunziza alishindwa kuheshimu mwafaka wa amani mbali na sheria za kimataifa. Wakati  Mapinduzi  hayo  yakitangazwa, Rais Nkurunziza alikuwa  nchini Tanzania kujumuika na viongozi wa kanda  ya Afrika Mashariki kutafuta suluhu ya mgogoro wa Burundi tangu Nkurunzinza atangaze nia yake ya kuwania awamu ya tatu. Baada  ya  tangazo  la  kupindulikwa  kwake, Rais  huyo  alipanda  ndege  kurejea  nchini  kwake  licha  ya  tangazo  la  kufungwa  kwa  mipaka  yote  na  viwanja  vya...

Diamond Amuita Jokate Makombo...."Mwacheni Ali Kiba Ajilie Makombo"

Mkali wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond’ amemuita mpenzi wake wa zamani Jokate Mwegelo kuwa ni makombo na kudai kama zilipendwa huyo anatembea na hasimu wake Ali Kiba, hakuna jipya kwani anakula makombo. Diamond ametoa kauli hiyo Jumatano iliyopita wakati mwanahabari wetu alipotaka kujua anajisikiaje kuona wapenzi wake wa zamani Jokate na Wema Sepetu ‘Madam’ wanamuunga mkono Ali Kiba. Pamoja na kudaiwa kuwa Jokate ana uhusiano wa ‘kimalovee’ na Ali Kiba na mwenyewe kutokubali, ameungana na Wema kuendesha kampeni ya nguvu kwenye mitandao ya kijamii kuhamasisha watu wampigie kura Kiba kwenye Tuzo za Kili 2015 kwa kile kinachoelezwa kuwa ni kampeni ya kuuangusha ufalme wa Diamond kimuziki. Baada ya mwanahabari wetu kuujua ‘mchezo huo’ uliopamba moto kama moto wa kifuu mitandaoni ndipo alipomuuliza Diamond anauzungumziaje ambapo kwanza alikiri kuufahamu na kudai ameudharau maana hauna jipya. “Hamna jipya waache waendelee kumpigia...

Gharama za kupima ardhi kupunguzwa

SERIKALI imesema katika mwaka ujao wa fedha itapunguza gharama za upimaji ardhi kwa zaidi ya nusu ili kuwawezesha wanachi kupima maeneo yao, hali ambayo inaonekana itapunguza migogoro ya ardhi. Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi wakati wa ziara mkoani hapa kwa ajili ya kutatua migogoro ya ardhi ambayo imedumu kwa miaka mingi. Akizungumza na watendaji wa sekta mbalimbali wa mkoa wa Tabora, Waziri Lukuvi alisema Wizara itapunguza kwa zaidi ya nusu, gharama za upimaji ardhi ili kila mwananchi aweze kupima eneo lake na kupata hati ya umiliki. Lukuvi aliongeza kuwa serikali pia itaweza kukusanya kwa wingi kodi ya pango la ardhi, hivyo kuongeza mapato ambayo yataisaidia serikali katika kufanikisha shughuli za maendeleo. Pamoja na kupunguza gharama hizo, Lukuvi aliwaonya maofisa ardhi kuacha tabia ya kuendesha shughuli za serikali kwa kukiuka taratibu, akitolea mfano wa maofisa hao kupima viwanja juu ya viwanja suala ambalo limekuwa lina...