MWAKILISHI wa Kudumu wa Umoja wa Afrika (AU) nchini Marekani, Balozi Amina Salum Ally amewataka viongozi wa Afrika kutumia mbinu mbalimbali ili kuziepusha nchi zao na migogoro ya mara kwa mara inayoweza kusababisha uvunjifu wa amani na kudumaa kwa uchumi.
Aliyasema hayo katika mahojiano maalum na kituo cha televisheni cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (Mlimani TV) juzi usiku alipokuwa akizungumzia masuala mbalimbali yanayohusu Bara la Afrika.
Alisema, baadhi ya nchi za Afrika zimekuwa katika wakati mgumu kukua kiuchumi kutokana na migogoro ya wenyewe kwa wenyewe kitu ambacho mbali na kupoteza amani iliyopo, kinahatarisha pia kukua kwa uchumi kwa mataifa hayo.
Ally alisema uchumi wa taifa lolote lile hauwezi kustawi ikiwa viongozi wake watashindwa kusimamia hali ya utulivu na amani.
“Wawekezaji wanapenda kuonawanawekezaji vitega uchumi vyao katika mazingira yenye amani na utulivu. Aliongeza: “Inashangaza kuona baadhi ya nchi za kiafrika zimekuwa zikitumia muda mwingi katika mizozo ya wenyewe kwa wenyewe, hali hii haiwezi kuvutia wawekezaji jambo ambalo linaathiri ukuaji wa uchumi wa bara hili.”
Ally ambaye amebobea katika masuala ya kiuchumi alieleza kusikitishwa kwake na hali ilivyo katika nchi ya Burundi na kusema kuwa kinachotakiwa kufanyika katika mazingira ya nchi hiyo na nyingine zenye migogoro ni watu kukaa chini na kuzungumza kwani hiyo ndiyo njia pekee ya kumaliza mizozo.
“Mimi naamini katika meza ya mazungumzo, ni kitu cha kawaida kuwa na mitazamo tofauti lakini mwisho wa siku ni vema kukubaliana kutokubaliana bila kumwaga damu ya mtu kwani siku zote mazungumzo ndiyo msingi wa taifa imara,” alisema
Comments
Post a Comment