MABINGWA wa Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu, Yanga, leo wanashuka dimbani kutafuta ushindi wa kunogesha sherehe za kupokea kombe lao katika mchezo dhidi ya Azam utakaochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Yanga wanatarajiwa kukabidhiwa kombe la ubingwa na mgeni rasmi katika mechi hiyo, Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk Fenella Mukangara baada tu ya kumalizika kwa mechi hiyo itakayoanza saa 11 jioni.
Tayari kikosi hicho cha Jangwani kina pointi 55, ambazo haziwezi kufikiwa na timu yoyote kwa sasa ambazo walizifikisha katika mchezo wao uliopita dhidi ya Polisi Morogoro baada ya kuwafunga mabao 4-1.
Timu wanayokutana nao, Azam FC yenye pointi 45 ndio yenye presha kubwa kwani wanahitaji ushindi katika mchezo huo ili kujiweka katika mazingira mazuri ya kuendelea kubaki katika nafasi ya pili.
Iwapo Azam itapoteza mchezo huo na ujao dhidi ya Mgambo Shooting ya Tanga itakuwa kwenye mazingira magumu ya kumaliza katika nafasi ya pili, lakini ikitoka sare au kushinda mchezo ujao, basi itakuwa imeinyima Simba nafasi hiyo ambayo wanaisaka kwa udi na uvumba ili kushiriki michuano ya kimataifa mwakani.
Kocha wa Azam FC, GeorgeNsimbe alisema anatarajia kikosi chake kitaondoka na ushindi katika mchezo huo. Nsimbe alisema ana imani kubwa na kikosi chake kinaweza kubadilisha matokeo na kuwa mazuri na hivyo kushika nafasi ya pili ili kushiriki michuano ya kimataifa mwakani.
Wakati Azam FC wakijitamba kushinda, Yanga ambao waliwasili juzi wakitokea Tunisia wamesema wamejipanga kuondoka na ushindi katika mchezo huo ili kusherehekea vizuri kombe lao.
Pia, imewakata kauli baadhi ya watu wanaotoa vitisho dhidi yao kuwataka iwafunge Azam FC, kuwa isiwapangie na kwamba iiwaache wafanye wanavyofahamu wao.
Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Yanga, Jerry Muro alisema jana kuwa kumekuwa na minong’ono na taarifa kwenye mitandao kuwa kuna dalili za kupanga matokeo, jambo alilosema halipo na wala hawatarajii kuwepo.
“Tusipewe vitisho vya kumfunga Azam FC, hatuko kumbeba mtu… mbona wakati tukihangaika kwa jasho letu hamkuwepo, hata hao mashabiki wa Simba ambao wanatafuta undugu, mbona kwenye mechi yetu dhidi ya Etoile du Sahel waliishangilia Tunisia, watuache wenyewe,” alisema Muro.
Alisema kitendo cha Yanga kuchukua ubingwa mapema isiwe ni tatizo kwani hawako kutumika kwa wengine. Alisema kocha aachwe mwenyewe atajua ni kikosi gani ambacho atakipanga na kwamba asipangiwe wala kuingiliwa na watu na wakati huo huo, akiomba mashabiki kujitokeza kwa wingi kushuhudia wakikabidhiwa kombe lao.
Mechi hiyo itachezeshwa na Jacob Adongo (Mara), akisaidiwa na Frednand Chacha (Mwanza), Hellen Mduma (Dar es Salaam), mwamuzi wa akiba Hussein Kalindo (Dar es Salaam) na Kamishna ni Damian Mabena (Tanga).
Kwa mujibu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), sherehe za makabidhiano ya tuzo zitaenda sambamba na wadhamini wa ligi, Kampuni ya simu za mkononi Vodacom kumkabidhi zawadi mchezaji bora wa Aprili, mshabuliaji wa Yanga, Mrisho Ngassa atakayezawadiwa Sh milioni moja
Comments
Post a Comment